Kimataifa

Harry Maguire: Tayari kwa Msimu Mpya na Man United

Harry Maguire: Tayari kwa Msimu Mpya na Man United

Harry Maguire, beki wa Manchester United na England, ameeleza kuwa bado yupo kwenye mipango ya timu kwa msimu ujao na yuko tayari kushinda mataji akiwa Old Trafford.

Msimu uliopita, Maguire hakupata nafasi ya kucheza mara kwa mara kutokana na majeraha yaliyokuwa yakimkabili, hali iliyomfanya acheze mechi 22 tu za Ligi Kuu England. Hivi sasa amesema yupo fiti na anasubiri kwa hamu kuitumikia timu hiyo katika msimu mpya. Beki huyo pia ameeleza kuwa amepewa uhakikisho wa nafasi yake katika timu, hivyo yupo tayari kupambana.

“Isipokuwa timu iniambie kwamba nipo sokoni au sihitajiki, lakini kwa sasa kutokana na mazungumzo niliyo nayo na vitendo vya timu, nina hakika nipo sehemu ya mipango ya timu. Sasa ni muda wa kupambana na kuhakikisha timu inafanikiwa na kushinda mataji,” alisema Maguire.

Maguire alipata jeraha la msuli mwishoni mwa msimu uliopita, hali iliyomlazimu kuwa nje ya uwanja katika fainali ya Kombe la FA na pia akakosa nafasi katika kikosi cha timu ya taifa ya England kilichoshiriki Euro 2024.

“Ulikuwa wakati mgumu katika maisha yangu ya soka. Nilikuwa najiandaa kwa ajili ya fainali ya FA na michuano ya Euro ili kuisaidia timu na nchi yangu, lakini niliishia kutocheza kutokana na majeraha,” alisema. Maguire ameungana na kikosi cha Manchester United huko Marekani kwa ajili ya maandalizi ya msimu mpya na atacheza mchezo wa kirafiki dhidi ya Arsenal wikiendi hii.

Leave a Comment