Soka

Simba na Yanga Waanza Kukabana Kuelekea Ngao ya Jamii

Simba na Yanga Waanza Kukabana Kuelekea Ngao ya Jamii

Wakati Yanga ikihitimisha Kilele cha Wiki ya Mwananchi jana, mashabiki wa Simba na Yanga walianza kutambiana kuelekea pambano la nusu fainali ya Ngao ya Jamii, litakalofanyika Alhamisi hii kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa. Tamasha hili linafuatia Simba Day iliyofanyika siku moja kabla ambapo mashine mpya za msimu wa 2024-2025 zilitambulishwa.

Simba na Yanga zinatarajiwa kukutana kwenye Dabi ya Kariakoo ya kwanza msimu huu, huku kila timu ikijivunia kuimarisha vikosi vyake baada ya matamasha yao maarufu. Katika mechi ya msimu uliopita, Simba iliibuka na ushindi wa penalti 3-1 dhidi ya Yanga kwenye Ngao ya Jamii, lakini ilipoteza mechi mbili kwenye Ligi Kuu kwa kuchapwa 5-1 na 2-1.

Mashabiki wa Simba wanaamini ni wakati muafaka wa kumaliza ubishi na wenzao, huku kila mmoja akiamini kikosi chake kipo tayari kufunika katika pambano hilo kabla ya kuanza kwa Ligi Kuu Bara Agosti 16. Mshindi wa mechi hiyo atakutana na mshindi wa pambano kati ya Azam na Coastal Union, litakalofanyika Agosti 8 kwenye Uwanja wa New Amaan Complex, Unguja.

Mashabiki wa klabu hizi kongwe wameanza kuchimbana biti mapema kabla ya pambano hilo kubwa, huku tukio la Yanga Kwa Mkapa jana likionekana kama kujibu mapigo kwa watani wao, Simba.

Leave a Comment